Thursday, November 13, 2008

Lazima tupande ndio tuvune. Yaani tuwekeze ndio tunufaike.

"Everyone wants to go in heaven; but nobody wants to die" Ni mameno ya Winston Hubert McIntosh ama Peter Tosh alipoimba kwenye Equal Rights. Kwa ufupi naona kama linalohimizwa hapa ni suala la kutaka kuweka bayana kuwa kama unahitaji chochote lazima kuwekeza gharama zitakiwazo.
Natazama "mfumo" wa serikali uliopo na najiuliza kama unatoa changamoto kwa watendaji kusaidia walio na uhitaji. Yaani kama Rais na wabunge wote wanachaguliwa kwa wakti mmoja ina maana ikitokea wabunge wakawa wengi kutoka katika chama cha Rais basi hata wasipotekeleza ilani za uchaguzi hakuna wa kuhoji kwa nguvu bungeni. Lakini pia najiuliza kama serikali ni kwa ajili ya wananchi si ina maana wanatakiwa wafanye kila lililo ndani ya uwezo wao kuwezesha wananchi kufanikiwa? Unadhani itawezekana kama kufanya kila liwezekanalo itamaanisha serikali kuhatarisha nguvu zake za kiutawala? Kimsingi tutasema NDIO lakini kiitifaki itakuwa HAPANA.
Lakini bado najiuliza kama tungekuwa na chaguzi tofauti, kwa maana Marais na wakuu wa mikoa wakachaguliwa miaka miwili na nusu kabla ya wabunge na madiwani si ingekuwa safi? Kwamba kwa nusu muhula tunawaangalia na kuwasoma viongozi waliopo madarakani na kama hawatekelezi lolote "tunawamwagia upupu" kwa kujaza wapinzani wao kwenye uchaguzi ujao. Ndhani hii ingeamsha UTEKELEZAJIwa ilani za uchaguzi na pia ingewasaidia wananchi kupata kile wanachohitaji kutoka kwa wawakilishi na viongozi wao.
Najua watasema ni gharama, lakini kama ndizo zitakazowasaidia wananchi kutoka kwenye umaskini na ujinga kwanini zisitumike? Kuna gharama gani zaidi ya kuwa na taifa lenye uhitaji mkubwa leo kama ambavyo ilikuwa miaka 37 iliyopita?
Gharama lazima zitumike kuokoa taifa maana NI LAZIMA TUPANDE NDIO TUVUNE, YAANI TUWEKEZE NDIPO TUNUFAIKE

No comments: