Monday, January 26, 2009

Wasanii wetu wanavyokuwa wasivyo

Ukisoma mahojiano yoyote ya msanii wa nyumbani (hasa kama ni ya kusifia) basi utakutana na sehemu ambayo msanii atajieleza kama KIOO CHA JAMII. Na mimi sina la kupinga juu ya mtazamo wao huo. Lakini pia nikiangilia jinsi wasanii wetu wanavyoonekana mbele ya jamii kutokana na matendo yao ndipo ninapoanza kupata shaka na KIOO wazungumziacho, ama wadhaniacho wanakiwakilisha. Tumesikia jinsi viongozi wa bendi mbalimbali walivyozungumza na Da Sophy wa Africa Bambataa blog juu ya kukerwa na tabia mbaya za matumizi ya madawa ya kulevya kwa wasanii wao. Hiyo ni baada ya mlolongo wa wasanii wa filamu kuhusishwa na mapenzi ya hovyo na picha za utupu (ambazo blog hii haiwezi thibitisha) lakini zikasambaa mtaani tena kwenye jamii ambayo wanataa iwachukulie kama kioo. Upande wa kile kiitwacho muziki wa kizazi kipya kumeendelea kuonesha kumomonyoka kwa ubunifu na kutoifaa jamii kwa kuendeleza nyimbo ambazo hazina ziifaacho jamii zaidi ya KUJITETEA, KUJISIFIA na KUENDELEZA MALUMBANO yasiyoifaa wala kuinufaisha jamii. Niliwahi kuandika Nov 11 kuhusu sanaa yetu ya BONGO FLAVA na nakumbuka nilisema kuwa iwe ni "bifu" kweli ama "game", ubunifu bado ni ziro na bado naendelea kuamini hivyo. Katika makala ama toleo la siku hiyo niliandika jinsi Inspekta Haruni alivyoimba kumjibu MwanaFa ambapo nilisema kwa asiyeelewa wimbo unaojibiwa hataelewa kinachoimbwa. Ni kama kilichotokea sasa ambapo MwanaFa na Jay Dee wameimba juu ya kusengenyana katika wimbo wao Msiache Kuongea unaoweza kuusikiliza kupitia Bongo Celebrity . Lakini bado naendelea kusema kuwa UBUNIFU ni ziro maana wameshindwa kutambua kuwa kusengenyana ni tatizo la jamii na si wao peke yao na wameimba wimbo mzima KUJITETEA na KUELEZWA NAMNA WANAVYOSONGA MBELE LICHA YA KUSEMWA huku wakionekana kuwalenga watu fulani. Naendelea kushangaa na kujiuliza namna waaminivyo wao ni "kioo cha jamii" ambayo hawataki kuitetea bali kutetea nafsi zao. Nina hakika wanatambua kuwa kusengenyana kupo na kumewaathiri wengi, na nilichotegemea ni kuwa baada ya wao kupata madhara ao wangeweza kuifikiria jamii inayosemwa na kusengenywa kila siku kisha wajiunge nayo kukomesha haya.
Ntarejea mifano niliyowahi kuitoa huko nyuma kuwa nani anajua kuwa wimbo wa Talaka Rejea, Msafri Kakiri, MV Mapenzi, Chatu Mkali na nyingine zilikuwa ni madongo kwa baadhi ya bendi? Na mbona kama hujui kuwa ni madongo unapata ujumbe halisi hata kama hauendani na yule aliyekuwa anafikishiwa ujumbe? Ndipo ninapowashangaa wasanii ambao wanashindwa kuweka mipaka ya hisia zao na mahitaji ya jamii. Ni kama wanaamua kuwa vioo vyao wenyewe na hapo ndipo ninapowashangaa. Ni katika "angle" hiyo ninapoona WASANII WETU WANAVYOKUWA WASIVYO yaani wakijiita vioo vya jamii ilhali wanaji-reflect wenyewe badala ya jamii.

Nawaacha naye Oliver Mtukudzi aliyeshirikishwa na msaniiwa kizazi kipya huko kwao wakisema Pane Rudo . Leo wala sitazungumzia umuhimu wa kutumia ala za asili katika muziki wa "kizazi kipya". Labda "Next Ijayo"




4 comments:

Anonymous said...

Mzee wa Changamoto nimeupenda huu uchambuzi wako katika suala hili.Hata mie huwa nashangaa huu usemi wa kioo cha jamii unaeleweka maana yake halisi au umekuwa tu msemo tu! Kuhusu Suala la ubunifu wow,hili bado mtihani kwa wengi ila nafikiri kujisomea ili kujua mambo mengi, kufanya research za kazi nzuri za wasanii,kujua umuhimu wa kutoa kazi original na sio kuiga,kujiendeleza katika hiyo taaluma ni baadhi ya mambo muhimu.

Anonymous said...

Mzee wa Changamoto nimeupenda huu uchambuzi wako katika suala hili.Hata mie huwa nashangaa huu usemi wa kioo cha jamii unaeleweka maana yake halisi au umekuwa tu msemo tu! Kuhusu Suala la ubunifu wow,hili bado mtihani kwa wengi ila nafikiri kujisomea ili kujua mambo mengi, kufanya research za kazi nzuri za wasanii,kujua umuhimu wa kutoa kazi original na sio kuiga,kujiendeleza katika hiyo taaluma ni baadhi ya mambo muhimu.

Unknown said...

Kwa wao usanii sio kioo cha jamii bali cha kujitazamia wao wenyewe na kujilinganisha na wengine.

Kaka Mubelwa naamini utakubaliana na mimi kwamba upeo mdogo wa elimu ndio kikwazo kikubwa kinachowakwamisha wasanii wetu.
Umezungumzia muziki wa bongo fleva, naomba uzitazame filamu zetu za bongo,uone vituko kama sio vioja.

Mzee wa Changamoto said...

Nashukuruni kwa maoni. Da Sophie naona umegusa ambacho pia Kaka Kaluse kasema. Kujisomea ili kujua mengi, kufanya chunguzi mbalimbali, kujitengenezea kazi zao binafsi na kujiendeleza kitaaluma ndio ELIMU ambayo Kaka Shaaban kasema. Kwa upande wa Filamu ndugu yangu kuna sehemu zatia kinyaa. Na ukweli ni kwamba sio kwamba hawaendelei, bali wanaendelea kukurupuka kutoa nyingine nyingi kabla hawajaklaa chini kuangalia na kurekebisha makosa ya zilizopita.
Kuna filamu ambazo ni aheri kuzisoma kwenye hadithi kuliko kuziona.
Lakini tutasonga tuuu