Wednesday, March 26, 2014

Jamii yaaswa kutowabagua watoto mfanano

Na Andrew Chale
JAMII imeaswa kutambua matatizo yanayowakumba watoto mfanano (mtindio wa ubongo) na kushauriwa kutokuwabagua. Aidha, wametakiwa kuachana na imani za kishirikina, kwamba watoto hao ni laana kutoka kwa Mungu na kuwaua, badala ya kutoa elimu kwa wanaowatenga watoto hao.
Mwenyekiti wa Chama cha watu wanaojitolea (Trabajo Voluntario), Marisa Yussuf Himid aliyasema hayo hivi karibuni jijini Dar es Salaam, alipokuwa kwenye ziara maalum ya kutembelea vyombo vya habari nchini.
Akiwa kwenye ziara hiyo aliweza kutembelea kampuni ya Free Media Limited ambao ni wachapishaji wa magazeti ya Tanzania Daima  na Sayari, na kujionea mambo mbalimbali ya kiutendaji ndani ya chumba hicho cha habari (Newsroom).
Displaying Kwa Mhariri wa Michezo.JPG
Mwandishi wa Gazeti la Tanzania Daima, Andrew Chale (kushoto) akimtambulisha Mwenyekiti wa Chama cha watu wanaojitolea (Trabajo Voluntario), Marisa Yussuf Himid  kwa Mhariri wa Michezo wa gazeti la Tanzania Daima, Tullo Chambo (katikati).
 Hata hivyo, Marisa ambaye alisema matatizo makubwa yanayowasumbua watoto hao ni kuingiliwa kimwili na wanaume au wanawake wanaotambua kuwa watoto hao hawana uelewa wa kutosha.
Pia alisema wanawake wengi wanaamua kuwafungia watoto hao ndani, kwani wengi wamewachukulia kama walemavu wa akili na kudiriki kuwabaka na kuwaambukiza Virusi Vya Ukimwi (VVU) kwa imani potofu kuwa jamii yao hiyo hawapati virisi hivyo.. (Hii si kweli ni upotoshwaji na vitendo hivi vikemewe na kuchukuliwa hatua kali dhidi ya wahusika).
“Tumeamua kuita kitengo hiki kwa jina la watoto mfanano kusudi kuondoa dhana ya watu kufikiri wana mtindio wa ubongo. Hivyo tumekuja kutoa elimu ya kwamba watoto hawa wana haki kama watoto wengine , tusiwabaguem” alisema Marisa.
Aliongeza watoto mfanano wanahitaji elimu kama watoto wengine na wapatiwe huduma za kiafya, ikiwa ni pamoja na tundu kwenye moyo, matatizo ya macho na upungufu wa vitamini na huduma nyingine.
Pia alisema katika kikundi chao walikuwepo watoto 45, lakini kutokana na elimu duni ya wazazi, watoto wengine walichukuliwa huku wengine wakifariki na hadi kufikia watoto 32.
“Mmoja wa wanasiasa na mwanakikundi hiki, Samia Suluhu anajiandaa kuleta walimu na madaktari watakaojitolea kuwasaidia watoto hao, kwani hadi sasa tumebaki na walimu watatu tu ambao bado wanaendelea kuwafundisha,” aliongeza.
Alisema kikundi hicho kinashirikiana na Taasisi ya Zanzibar Association of Downsyndrome Children (ZADOC) kwa kuwakusanya na kuwapatia mafunzoa watoto hao kwa kipindi cha miezi sita.
Aliongeza kikundi hicho kilianza mwaka 2005 kwa kuhamasisha wananchi kujitolea zaidi katika kuwalea watoto mfanano na kuhamasisha jamii kuwatambua.

No comments: