Showing posts with label Uchaguzi 2015. Show all posts
Showing posts with label Uchaguzi 2015. Show all posts

Thursday, October 6, 2011

NIONAVYO MIMI. Wapinzani "WAJISEME" kabla "HAWAJAWASEMA"


Wiki hii tumeshuhudia kwa mara nyingine "USHINDWI" katika siasa huko Igunga. Nazungumzia kwenye uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Bw. Rostam Aziz ambaye aliamua kujiuzulu nyadhifa zake ukiwemo ubunge. Kwa bahati mbaya, WOTE WALIOSHIRIKI WALISHINDWA (kwa mtazamo wangu) kuifanya siasa kama chombo cha kuihudumia jamii badala yake wakaugeuza uchaguzi huo kuwa NGAZI YA KUPATIA MADARAKA.
Ni harakati hizi zilizoleta mambo mbalimbali kuwezesha harakati za kukwaa madaraka hayo. Tumeshuhudia helikopta, fedha, "majeshi" na kila nguvu zikipelekwa Igunga kwa wiki chache ili kupata KITI hicho cha ubunge. Ni kwa mantiki hii nilipoandika kwenye ukurasa wangu wa Facebook kuwa "Mshindi kashindwa na mshindwi kashinda. Nani ni nani na ni nani aonaye ushindi wa sasa kama ushindwi ujao naye aonaye ushindwi wa sasa kama ushindi ujao? Ni LAZIMA SIASA ZETU ZIWE ZAIDI YA KUSHINDA NA KUSHINDWA. Ziwe UTUMISHI KWA UMMA.
Nasubiri kuona ni wangapi waliokuwa Igunga wiki kadhaa zilizopita watarejea "kuwajulia hali" kabla ya 2015.
Nawaza kwa sauti tuuu!!!!"

Ninalowaza ni kuwa katika uchaguzi huu wa "vuta nikuvute", na ulioshuhudia "MAJESHI" ya aina mbalimbali, ni kiasi gani cha pesa kimetumika huko? Na ni kweli kuwa matumizi hayo yataendana na kasi ya maendeleo kwa wana Igunga? Ni kweli kuwa chama tawala kimeshutumiwa na kutuhumiwa kutumia pesa na kila rasilimali iliyo ndani ya uwezo wao, lakini je, UPINZANI mmefanya nini kusuia hili lisitokee wakati ujao? Sote tumesikia matokeo [kuwa Dk. Kafumu alishinda kwa kura 26,484 sawa asilimia 50.56, mgombea wa Chadema, Joseph Kashindye, alipata kura 23,260 sawa na asilimia 44.32 wakati mgombea wa CUF, Leopard Mahona, aliambulia kura 2,104 sawa na asilimia 4.01.)Stephen Mahui wa AFP (235), Hassan Lutegeza wa Chausta (183), Said Cheni wa DP (76), John Maguma wa Sau (83) na Hemed Dedu wa UPDP (63)]
Ninalowaza ni namna ambavyo MUUNGANO WA WAPINZANI (ambao wote wanaigiza kuwa na nia moja ya kuing'oa CCM) ungeweza kuwa suluhisho (kama sio tishio halisi) kwa chama tawala. Na nia hapa si kukitisha chama kuwtwaa madaraka yake, bali kutisha kuwa kisipowajali wananchi kitakosa ama kupoteza viti vingi.
Ni kwanini hata apataye kura 63 aamini kuwa anaweza kuibadili Igunga peke yake? Kwanini asiwekeze kwenye kuvishawishi vyama kumsomamisha yeye, ama atumie kura zake 63 kuwahamasisha wengine kumpigia mmoja watakayekuwa naye?
UPUNZANI......Mna miaka minne kusawazisha haya. Sote tunajua kuwa upinzani hauko sawa nchi nzima. Ni lazima tukumbuke kuwa kuna baadhi ya sehemu ambapo vyama fulani vyakubalika kuliko kwingine. Ni kwanini chama kisicho na wafuasi wengi mahala fulani kuliko kwingine. Ni kwanini vyama hivi visisimamishe mgombea mmoja kwa mujibu wa kukubaliana walikonako? Ukweli ni kuwa bila muungano hakuna ushindi.
Narejea nilichowahi kusema kuwa "JAPO DALILI ZA MTI KUKOSA MAJI TWAZIONA KWENYE MATAWI / MAJANI, LAKINI WAKATI WA KUTATUA TATIZO HILO HATUMWAGILII MAJANI BALI MIZIZI". Ni ujinga kwa wapinzani kuamini kuwa wanaweza kuleta mabadiliko nchini Tanzania kwa kutwaa nafasi za ubunge na uRais pekee (ambao wote si watendaji wa wananchi nchini mwetu). Naamini ni wakati ambao wapinzani wanatakiwa waanze SAFARI KUELEKEA MASHINANI kueleza sera zao ambazo sina hakika kama wengi wanazijua.
Ni wakati ambao hakuna "danganya toto" ya wasanii, wala kikundi fulani. Hakuna kanga wala kofia wala sukari. Ni wakati ambao utamkuta mtu asiye na munkari wa helikopta ana anayepekeshwa na hisia za kumuona "nyota" fulani. Ni wakati huu ambao wanatakiwa kwenda kwa wananchi KAMA WAO, bila mbwembwe za HELIKOPTA na kwa kuwa kama wananchi na kuwakuta katika fikra tulivu, wataweza kuwaelimisha juu ya kile wanachopanga kufanya, kuhusu ilani zao na mipango yao na kisha itawawia rahisi KUWAELIMISHA NA KUWAELEWESHA wananchi juu ya kile wanachopanga kufanya kwa kutumia ama kupitia sera zao. Na hili ndilo ambalo WANANCHI WANAKOSA. ELIMU JUU YA MAANA, NGUVU NA THAMANI YA KURA ZAO. Narejea kunukuu "status" yangu nyingine kwenye Facebook kuwa "TANZANIA HAITABADILIKA iwapo wananchi hawajui / hawatajua MAANA, NGUVU NA THAMANI YA KURA ZAO. Iwapo hawatajua kuwa KURA NI MAKUBALIANO / MKATABA wa KUSHIRIKI katika kutekeleza (na si kukaa kutekelezewa) ahadi ambazo mgombea amezitoa. Iwapo hawatajua kuwa KURA SIO MAZOEA YA CHAMA na kuwa SI LAZIMA IENDANE NA UANACHAMA BALI SERA ZA MGOMBEA NA MAHITAJI YAO na kuwa wanaweza kumpigia kura mgombea wa chama kingine na hata kuchagua Rais, Mbunge na Diwani toka vyama tofauti KULINGANA NA SERA NA MIPANGO YA KUTEKELEZA MAHITAJI YAO.
Nawaza kwa sauti tuuu!!!!"
Novemba 4 mwaka jana niliandika kuwa AJENDA KUU YA UCHAGUZI 2015 IWE UCHAGUZI 2010. Na sasa ni wakati ambao wapinzani wanatakiwa kukaa chini na KUJIANGALIA UPYA. Kuangalia mipango yao na namna ambavyo wataifikisha na kuielewesha kwa jamii. Kuangalia NIA YAO KAMA WAPINZANI na pia kama vyama vya upinzani, kisha kuchuja washirika na wasio washirika na hapo watapata la kufanya kwa manufaa ya wananchi. Si lazima wao wachukue nchi, lakini "kuwatia jambajamba" watawala itatosha kuwa utumishi. Lakini KWANZA WAMALIZE MGAWANYIKO ULIOMO NDANI MWAO kabla hawajafikiria KUWASEMA WALIO CHAMA TAWALA kwa yale watendayo. Na ndio maana nasema NIONAVYO MIMI. Wapinzani WAJISEME kabla HAWAJAWASEMA

Na huu ni MTAZAMO WANGU kwa namna nionavyo tatizo. Natunza haki zote za kukosea na kukosolewa kwani yawezekana kuwa NAMNA NIONAVYO TATIZO NDIO TATIZO

Tuonane "Next Ijayo"

Thursday, November 4, 2010

AGENDA YA KWANZA YA UCHAGUZI WA 2015 IWE NI UCHAGUZI WA 2010

"A nation that forgets its past is doomed to repeat it." Sir Winston Churchill
Nilipobandika toleo langu la kwanza la kipengele cha "UCHAGUZI 2010" la Machi 11, 2009 nilipata barua pepe ikiniambia kuwa "uchaguzi ni mwakani wewe unaanza kuujadili sasa?". Naamini alilomaanisha mtuma ujumbe ni kuwa nilikuwa nimewahi mno kuanza kujadili mchakato mzima wa uchaguzi kwani bado kulikuwa na mwaka mmoja, miezi saba na siku 20 kabla ya "siku ya siku". Lakini sasa.... ni historia.
Uchaguzi mkuu wa Tanzania ndio umemalizika kwa wananchi "kutuma ujumbe" kwa wahusika kwa namna waliyoamini ni sahihi. Lakini wakati uchaguzi huo ukisubiri matokeo (ambayo naamini "yanawekwa sawa" kabla ya kutangazwa), naamini pia HUU NDIO WAKATI WA KUANZA RASMI MBIO ZA 2015 KWA WENYE NIA DHAHIRI NA HALISI YA KUIKOMBOA TANZANIA.
Ninasema mbio zianze kwani ni vema kwa wahusika kuanza kutengeneza mazingira mazuri ya uchaguzi kwa kujaribu kukosoa mambo mbalimbali yaliyojitokeza katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Na kama matokeo ya jumla kwa nchi kama Tanzania yanaweza kuchukua siku kadhaa "kuwekwa sawa" na kutangazwa, naamini KUBADILI MFUMO WA UCHAGUZI KUTAHITAJI MIAKA KADHAA.
Ni katika kuwaza namna ya KUBORESHA uchaguzi wa mwaka 2015, nikaona kukusanya haya machache ambayo nayaona kama ajenda / agenda ya kwanza katika kuelekea uchaguzi huo ili wakati ukifika tusirejee "kulia" kwa yale ambayo yalishatokea na tukayapuuza. Na ndio maana nilianza na hiyo nukuu ya Sir Churchill.
Sasa baadhi ya ajenda za CHANGAMOTOYETU kuelekea uchaguzi 2015 ni.....
1: MIDAHALO KWA WAGOMBEA URAIS NI LAZIMA.
Mwaka huu nilishangazwa, kusikitishwa na kukereka na namna ambavyo chama tawala kilionesha dharau kwa kugoma kufanya mdahalo. Sababu niliyoisikia ikitajwa ni kuwa wagombea watawafuata wananchi huko waliko. Huu ni upungufu wa elimu ya awali ya uraia.
Kuna haja kwa bunge kupitisha SHERIA ya midahalo (japo mitatu) kwa wagombea wote wa nafasi ya uraisi ili kuweza kuwapa uwanja wa kupambana. Mwaka huu tumeona walivyokuwa wakirushiana "ya nguoni" kwa kuwa tu hawakuweza kukabiliana ana kwa ana kupambanisha sera.
2: REJEO ZA AHADI ZA UCHAGUZI 2010
Sitashangaa kusikia kuwa ni asilimia chache ya waTanzania wanajua nani aliahidi nini wakati wa kampeni. Hili ni kwa kuwa siamini kama kila aliyejitokea na fulana ya chama huzika alikuwa amekwenda kusikiliza sera na si kingine. Baadhi ya wagombea wameonekana kwenye taswira wakiwa na umati wa kuridhisha japokuwa si hakika kuwa wote walioenda walisikia na kunukuu ahadi zilizotolewa. Kama hukubahatika kuziweka ktk kumbukumbu, ZISOME (za wagombea uraisi) HAPA
Kinachotakiwa ni kusubiri 2015 ili kujua zimetekelezwa vipi.
3: UCHAMBUZI WA AHADI ZINAZOTOLEWA.
Kwa bahati mbaya ni kuwa wengi wa "waandishi" wanawekeza kwenye kunukuu kilichosemwa na si kusaka uhalali wa kinachosemwa. Mfano, nilimsikia mgombea uRaisi kwa CCM akisema... ndani ya miaka 5 atahakikisha maji toka ziwa Victoria yanawafikia watu wa Tabora ilhali walio "mwaloni" katika mikoa ya Mwanza, Kagera na Mara hawana maji ya kutosha toka ziwa hilohilo ambalo lipo mwendo mfupi zaidi ukilinganisha na mkoa wa Tabora. Watu wakapiga makofi, vigelegele na naamini kura zikahahakishwa...Hakuna aliyehoji wala kudadisi usahihi wa ahadi kama hiyo na kuwa kama atafanya hivyo kwa Tabora baada ya kumaliza Kagera Mwanza na Mara.
4: KAMPENI SI NYUSO ZA WATU PEKEE.
Helikopta zilikuwa kivutio kikubwa saana (na pengine ukiongeza fulana, kuwaona wasanii bure, kofia, kanga na kadhalika..) vyaweza kuwa sababu pekee ya watu kufurika mikutanoni. Lakini swali hapa ni kuwa ni kwanini wagombea wahimize kuona maisha ya wananchi mikutanoni? Nina hakika kuna mahali ambapo wagombea wa mwaka huu hawatarejea tena mpaka miaka 5 ijayo watakapoomba kura. Je! ni asilimia ngapi ya matatizo ya wananchi hudhihirika kwenye mikutano ya kampeni?
Kuna haja wagombea wakatafuta namna ya kuungana na kujihusisha na maisha halisi ya wananchi kwa kuwatembelea na kuona mazingira waishiyo hivyo usafiri usiwe wa kupaa na kutua pekee. Labda ndio maana wagombea hawajui hata kero za barabara za "wananchi wao".
5: TUME YA UCHAGUZI.
Hapa najua sina la kunena. Hii ya mwaka huu imenifurahisha zaidi maana licha ta TEKNOLOJIA kutumika katika chaguzi za miaka hii, licha ya kuwa tume hii ilikuwa ikitambua na kujiandaa kwa uchaguzi huu tangu mwaka 2005 (ulipoisha uliopita), licha ya wagombea kusema miundombinu imetengemaa zaidi, bado tume ya uchaguzi imekuwa kero zaidi ya maelezo.. Hili wengi walilizungumzia na hata mtandao wa Bongo Celebrity uliliongelea.
Kwa ujumla TUME YA UCHAGUZI TANZANIA INASTAHILI MAREKEBISHO.
6: ELIMU YA URAIA KWA WANANCHI
Kati ya mambo yaliyosikitisha katika uchaguzi uliomalizika ni idadi ndogo ya waliojitokeza kupiga kura ukilinganisha na waliojiandikisha. Na pia kura zilizoharibika zimekuwa nyingi kiasi kwamba kama uharibifu huo ungezuiwa kwa elimu ya uraia kwa wapiga kura, labda matokeo yangekuwa tofauti na yalivyo. Mfano halisi ni nafasi ya Uraisi visiwani Zanzibar ambapo tofauti kati ya Rais Ali Mohamed Shein na aliyeshika nafasi ya pili, Seif Sharif Hammad ilikuwa ni kura 3471 ilhali zilizoharibika ni 6109. Kwa maana nyingine, kama theluthi mbili ya kura zilizoharibika zingeweza kuwa halali, kungekuwa na ushindi mpana ama wa tofauti zaidi.
Lakini yote juu ya yote, kusikia kitui kiliandikisha watu elfu ishirini na waliopiga kura ni elfu tatu hizi si habari za kupuuza hata kidogo.
Unahitajika uelimishaji kwa wapiga kura ili watumiapo muda wao (ambao wanatakiwa kuhimizwa kuutumia) kupiga kura, basi wahakikishe kuwa kura zao haziharibiki na uchaguzi wao unahesabika.

Uchaguzi 2015 ni "label" inayozungumzia namna nilivyoona uchaguzi wa 2010 na namna niionavyo nchi yangu ya Tanzania ijiandaavyo na uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015. Kwa maandishi mengine juu ya mada hii katika "label" hii BOFYA HAPA