Thursday, January 14, 2010

Niangaliapo HAITI naiona TANZANIA

Image from CreativeCOW.net
Nimesikitishwa saana na yaliyotokea HAITI. Nchi yenye uhitaji ambayo sasa imekumbwa na tatizo asilia la tetemeko la ardhi. Tetemeko hili limeukumba mji mkuu na ulio na wakazi wengi zaidi nchini humo wa Port-Au-Prince. INASIKITISHA
Lakini tunapoangalia kilichotokea twajifunza nini? Twajiandaa vipi kwa matatizo kama haya kwa nchi yetu ya Tanzania?
Kuna mambo ambayo nayaona HAITI sasa ambayo yananifanya nijiulize kuhusu Tanzania yangu
Kwanza ni idadi ya waathirika wa tetemeko hilo ambayo ni kubwa saana. Idadi hiyo ya waathirika inatokana na idadi ya watu ndani ya mji wa Port-Au-Prince ambayo inaonesha harakati za wananchi kusaka maisha mijini kutokana na mgawanyo m'baya wa rasilimali, vitendea kazi na miundombinu nchini humo.
HILI NDILO LILILOPO TANZANIA.
Tukumbuke kuwa Tanzania (na hasa Dar Es Salaam) iko katika hatihati ya kukumbwa na athari za ongezeko la kina cha maji na ilionja athari za Tsunami japo haikuwa na madhara. Sasa nawaza................
Hivyo "vikwangua anga" ninavyosikia "vinaota" kila siku vimejengwa kuweza kuhimili matetemeko ya ardhi ama ndio mwendo wa "kitu kidogo" tusonge? Na ziliishia wapi tetesi za kupinda kwa jengo la Mafuta House? Ni kweli kuwa majengo yote yanayojengwa sasa jijini ni salama na yanafikia kiwango cha kuhimili athari kama haya?
Kwa mji kama Dar Es Salaam, kuna urahisi gani wa waokozi kuwafikia watakaokuwa matatizoni iwapo litatokea? Kama majengo ndio haya (ambayo ubora wake hatuujui) na barabara hazipanuliwi wala kuboresha mfumo wa usafiri wa ardhini, ni vipi tunajiandaa kiuokozi kwa matatizo yasiyoepukika kama hili lililotokea Haiti?
Na tunaweza kuwa na hata KISIO (estimation) ya wakazi waishio kwenye miji mikuu nchini mwetu?
Tanzania yangu ya sasa inajaza mamilioni ya vijana na wasaka maisha mijini kwa kuwa kuna mgawanyo mbaya saana wa rasilimali na miundombinu.
Vijiji vilivyo na ardhi zenye rutuba havina wakazi kwa kuwa wakazi wamechoka kulima na kisha KUKOPWA na serikali na wengine kushindwa kuuza mazao yao kwa kuwa hakuna mnunuzi. Huduma za jamii kama Barabara, Maji safi, Umeme, huduma za afya n.k zinakuwa kama anasa kwa waTanzania ilhali sasa ni mahitaji muhimu kusonga mbele na pengine "haki" kwa wananchi. Na athari za kutokamilisha miundombinu vijijini ndio haya ya watu wote kurundikana mijini na hata kama hakuna huduma za kuwatosha wote.
Mfano halisi ni mwaka 2003 ambao nilikuwa wilayani Karagwe. Nilishuhudia watu wakitelekeza mikungu mikubwa ya ndizi kwenye magulio kwa kuwa hakukuwa na wa kununua. Yupo aliyekuwa akitafuta wa kubadilishana naye kwa pakiti ya chumvi (ya sh 50/= wakati huo) na hakumpata. Hakuna anayenunua ndizi kwani kila mmoja zamuivia njiani na hakuna wa kuzipeleka Bukoba mjini ziende Mwanza na kwingine kwenye uhitaji kwa kuwa barabara haipitiki kwa gari la mizigo. Mkungu huohuo wa ndizi uliokuwa unaozea gulioni Karagwe unauzwa maelfu ya shilingi mjini Bukoba na makumi ya maelfu Mwanza na Dar. Bado serikali ikaja na "danganya toto" ya kusamehe kodi kwa wananchi. Nililowaza ni kuwa ni wangapi wako tayari kulipa kodi kama wantaweza kufanya mauzo ya ndizi zao? Kama kodi yenyewe ni shilingi 5000/= na watu wanapoteza makumi ya maelfu kwa kuwa hawawezi kuuza ndizi zao, kwanini wasikimbilie Dar na miji mingine kuangalia ustaarabu wa maisha? Bado ndugu zangu pale kijijini kwetu wanalima kahawa na kuishia KUKOPWA na serikali na malipo yao yanakuja miezi kadhaa baadae.
Ni nani anayechochea watu kurundikana mijini?
Ni nani wa kulaumiwa kwa mgawanyiko huu wa mji na vijiji?
Ni vipi tutaweza kuwaelimisha viongozi wetu watambue kuwa nao ni chanzo?
HEAVEN HELP US ALL

Tanzania Yangu ni kipengele kinachozungumzia ytale yaendeleayo nchini Tanzania na namna ambavyo "ndivyo sivyo" inavyozidi kupamba moto nchini. Kwa matoleo yaliyotangulia BOFYA HAPA
Tuonane "Next Ijayo"

4 comments:

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

mungu hepushi mbali jamnga kama hili jijini Dar. yasani ikiykea itakuwa soo. majengo yalivyojengwa hata likikatiza dege kubwa majengo hupata nyufa!

anyway katika tanzania matetemeko hupitia mitaa ya Kigoma, sumbawanga, mbeya, kagera kidogo lakini sio Dar, ila ikijatokea weweweeewewewewewew

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

duh!

tatizo ni kuwa tuna vichwa vigumu kuliko kamongo :-(

halafu hatuna mipango madhubuti kujiandaa na maafa... :-(

Yasinta Ngonyani said...

Unajua tatizo ni kwamba tunajisahau kabisa kwa vile tunajua Tanzania yetu ni nchi ya amani ni kweli ni nchi ya amani. Lakini hata hivi inabidi tujiandaa kwa kila jambo kwani popote pale linatokea. Angalia huko yakotokea tusidhani kuwa wao wanaombea yatoke hayo yanayotokea hapana. Munge ibariki Tanzania yetu na pia zibariki nchi nyingine zote.Upendo daima!!

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

@Yasinta: una uhakika tuna AMANI?