Wednesday, May 22, 2013

Tanzania Yangu.....Inayotunza "ubongo wa digitali" ndani ya "fuvu la analogia"

Photo Credits: Cafepress.com
Dunia ya sasa imefikia wakati ambao ni vigumu saana kudhibiti usambaaji wa habari popote na kwa yeyote.
Sasa hivi, ni kama DUNIA IKO VIGANJANI MWA WANANCHI hata walio mbali na "makao makuu" ya taarifa mbalimbali.
Walio vijijini wanajua kinachoendelea upande wa pili wa dunia bila kufika huko. Ni kwa kuwa simu za "nununu" zinauweka ulimwengu mikononi mwao muda wowote.
Kwa maana nyingine, NI NGUMU KUPUMBAZA walio kwako kwa kuwa wanapata zaidi ya kitokacho kwako.
Nirejee kwa viongozi wetu....
Utawasikia viongozi wakisema "msifananishe hilo la Marekani na hapa Tanzania kwa kuwa wao (Marekani) wamekuwa huru kwa miaka 200 wakati sisi tumekuwa huru kwa miaka 50 tu"
Lakini...wanapopata pesa za kununua MASHANGINGI, hawanunui ambayo Marekani walitumia wakati wa miaka 50 ya uhuru wao
Wanalazimisha watu kuishi maisha ambayo hayaendani na wakati  (katika yale yanayohusu uwajibikaji wao) na kupuuza hilohilo katika yale yahusuyo wananchi.
Kumekuwa na ile DHANA YA KUTAWALA WANANCHI KWA UKOSEFU WA TAARIFA SAHIHI KWAO (wananchi) na hilo linaanza kuwa kikwazo kwa watawala hao kwa kuwa wananchi wanapata habari toka vyanzo mbalimbali duniani (japo wakati mwingine hili linakuwa na madhara makubwa)
Yaani tuna viongozi wanaoamini kuwa wanaweza kuwazuia wananchi wanaoishi na kuwa katika mfumo wa kiDIGITALI kuenenda sawa na "dunia iliyo viganjani mwao" kwa mbinu zao za kiANALOGIA ambazo zinahusisha NGUVU KULIKO TAARIFA ZINAZOKOSEKANA NA KUHITAJIWA NA WANANCHI.
Kumekuwa na tatizo la TAARIFA kwa wananchi kutoka serikalini mwetu na blogu hii imekuwa ikililalamikia sana.
Kinachoonekana ni kuwa WANANCHI WANALAMIMIKIA MAMBO AMBAYO WENYE UFAHAMU NAYO WANAWAONA KAMA VITUKO na hii ni kwa kuwa wananchi wengi hawapati taarifa kamili ya kile kinachoendelea ilhali wenye taarifa kamili wameKAA NAZO.
Sasa tunaona maafa ya wananchi kuchukua hatua wanapohisi wanapuuzwa, ilhali maamuzi yanakuwa yameshafanywa na walitakiwa kujulishwa.
WANAJIONA WANAPUUZWA.
Labda niwakumbushe WATAWALA wetu kuwa katika ulimwengu wa sasa, huwezi kuwafunga wananchi kujua kinachoendelea duniani kwa kuwa DUNIA YA SASA NA UKUBWA WAKE IKO VIGANJANI MWA WATU
Watawala wetu wamewekeza katika "kujenga UKUTA wakiamini itaweza kuzuia HARUFU".
Wanashindwa kuripoti uhalisia wa mambo yanayotokea wakiamini watu hawatapata taarifa kamili na watu wanapogundua kinachoendelea wanahisi KUPUUZWA na / ama kudharauliwa.
Ukweli ni kuwa, ulimwengu wa sasa si wa kutawala watu kwa mabavu na kupuuza nguvu ya mawasiliano ya kiDIGITALI yaliyo kila mahali kwa kutumia njia / mbinu za kiANALOGIA.
Ni LAZIMA WATAWALA WAKUBALI kuwa wanaongoza watu ambao tayari wamesonga mbele kifikra. Na hivyo ni busara nao kusonga nao vivyo hivyo.
Kwa tafsiri yangu, FUVU ndilo linalokinga ubongo.
Na sasa wanaotukinga waTanzania ni VIONGOZI ambao hawataki kuendana na mazingira ya sasa ya dunia.
Yaani....
Yawezekana hata sasa wapo viongozi wanaoshangaa kuona kuna VIONGOZI "WAZEE" wenye akaunti kwenye social media bila kutambua kuwa kwa kufanya hivyo WANAJIFUNZA kile ambacho wananchi wanakijua kwa usahihi ama kinyume chake na kwa kutambua TATIZO, inakuwa rahisi kulikabili.

Tunajua kuwa maandamano na vurugu zilizosababisha mapinduzi makubwa katika nchi kama MISRI na LIBYA hayakuandaliwa kwa mikutano ya hadhara, bali mitandao ya kijamii, hivyo kujua nini wanaelewa na wanaamini ni njia gani ya kutatua matatizo yao, kunaweza kukufanya ukajipanga vema KUWAELEWESHA WASICHOELEWA NA KUWASAIDIA KUTAFUTA NJIA M'BADALA NA YA THAMANI KATIKA KUSAKA HAKI YAO
Ina maana.....

UBONGO (wananchi) umeshafikia kiwango cha DIGITALI cha kupata karibu kila wanalotaka kwenye mtandao, na kusaidiwa kuamua watakavyo kwa kujisomea kupitia mitandao, lakini maFUVU yetu (viongozi) bado yanaamini katika MIKUTANO YA HADHARA ambayo kwa bahati mbaya haina mvuto, haikusanyi watu wengi na haifanyiki kwa wakati muafaka wala kuwafikia kwa haraka kama habari za mitandaoni.
NAAMINI (viongozi) WANGEANZA KWA KUSAMBAZA HABARI SAHIHI KWA NAMNA NA MWENDO ULEULE AMBAO HABARI ZISIZO SAHIHI ZINASAMBAA ILI KUHAKIKISHA KUWA WANA-MATCH MWENDOKASI WA UTOAJI WA TAARIFA AMBAO "UBONGO" (wananchi) WANAO

UKWELI NI KUWA....
Viongozi wetu wanastahili kuji-update katika fikra na kauli zao ili kujua namna ya kuenenda na kasi ya mabadiliko ya teknolojia yanayowawezesha wananchi kujua kinachoendelea duniani kote pale yanapotokea. 
Lakini hii ndio Tanzania yangu....Inayotunza "ubongo wa digitali" ndani ya "fuvu la analogia"



Tanzania Yangu ni kipengele kinachozungumzia ytale yaendeleayo nchini Tanzania na namna ambavyo "ndivyo sivyo" inavyozidi kupamba moto nchini. Kwa matoleo yaliyotangulia BOFYA HAPA
Tuonane "Next Ijayo"

1 comment:

emuthree said...

Mkuu hapo kwa sasa siongezi kitu, bali nasema tupo pamoja,