Thursday, July 16, 2009

MTAZAMO: Pale tunapochochea Rushwa, Ufisadi na Ubadhirifu

Oktoba 23 mwaka jana niliandika kuhusu mtazamo wangu wa Pale tunapochochea ujinga (Bofya hapa kuisoma) na kuwa lilikuwa namna ambavyo SERIKALI inaona namna ambavyo ujinga unavyoendekezwa nyumbani bila kuchukua hatua yoyote.
Lakini pia katika miaka ya karibuni tumeshuhudia baadhi ya waliokuwa wafanyakazi WAADILIFU wa serikali wakiishi maisha ya dhiki na ombaomba kana kwamba walifanya makosa kutii uadilifu. Na sasa tunashuhudia namna ambavyo wafanyakazi wastaafu wanavyohangaika kufuatilia mafao yao kwa zaidi ya nusu mwaka na bado wasipate sehemu ya kutosha ya mafao yao. Nimesoma kuhusu wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao kwa miongo sasa wamekuwa wakifuatilia mafao yao bila mafanikio kiasi cha kuishitaki serikali kwenye Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa
Sina hakika na malimbikizo ya malipo ya mishahara ya wabunge na WATAWALA wengine kama iko na inachukua muda mrefu kama ilivyo kwa WANYONGE HAWA.
Nimekuwa nikijiuliza kuhusu UKUBWA wa Wizara zetu kiasi cha kuyafanya "mafaili" kutoonekana kwa miezi yote hiyo na kinachowakuta wale ambao wanatoka mikoani kufuatilia mafao hayo wakiwa hawana mahala pa kuishi zaidi ya kupanga.
Sishangai namna ambavyo wafanyakazi wa serikali"wanavyojiwekezea mapema" kwa kuomba na kupokea Rushwa, kuiba na kujilimbikizia kile wawezacho kwa kuwa nao (kama ambavyo ingekuwa kwa wengi) hawataki kufikia wakati wa kustaafu na kuishia kuhangaikia mafao kwa pilika sawa na walizotumia wakati wa kutafuta maisha.
Na ndio maana nasema KAMA KILIO HIKI KIMEKUWA KIKISIKIKA KWA MUDA WOTE HUU NA HAKUNA ANAYEONEKANA KUSHUGHULIKIA, BASI NA SERIKALI YENYE DHUMUNI LA KUZUIA AMA KUEPUSHA MATESO HAYA INA SEHEMU YA LAWAMA NA NDIO MAANA NAONA NAYO INAHUSIKA KATIKA KUCHOCHEA HAYA (kwa kuwa haifanyi kazi yake ya kuzuia kutokea)
Kwa hakika ni kama KILIO CHA SAMAKI.

1 comment:

Yasinta Ngonyani said...

Nimekuelewa, Na nionavyo mimi ni viongozi ndio wa kuwalaumu kwa vile wao ndio wanaopokea rushwa. Kuhusu mafao ya wastaafu, inasikitisha sana kwa kweli kwa mfano baba yangu amestaafu mwaka 2007 na ni mwei uliopita tu ndo kapata mafao yake amesumbuka sana. Yaani ameitumikia serikali halafu sasa kachoka lakini wao hawaoni hilo. Kwa nini wasiwaache wazee wapumzike kwa raha? Ni mtazamo wangu tu....