Wednesday, April 14, 2010

Vigezo vya Utoto, Ujana na Uzee ni vipi?

Siku chache zilizopita nilikuwa nikiwasiliana na rafiki yangu mmoja ambaye tumekuwa tukiwasiliana kwa muda kupitia blog na facebook. Mawasiliano ya sasa yalikuja siku chache baada ya kuwa nimebadili picha yangu ya ukaribisho kwenye blog na ukurasa wa mbele wa Facebook na hilo lilimfanya aingie kwenye ukurasa wangu wa taswira na kuanza kuzipitia.
Rafiki huyu ambaye amekuwa akisoma maandishi yangu ya hapa kwa muda mrefu, aliniomba radhi kisha akaniuliza "hivi kaka una umri gani (kama hutojali mimi kukuuliza) na nilipomtajia akashangaa na kucheka. Kisha akasema kwa muda woote aliokuwa akisoma maandishi yangu, alikuwa akinibashiria miaka 45 na zaidi. Lakini alishangazwa kujua alikuwa kanikuza kwa zaidi ya muongo na nusu.
Sikuwaza saana siku hiyo mpaka juzi nilipokuwa napitia taswira mbalimbali kisha nikakutana na moja niliyopiga na wafanyakazi wenzangu wa 100.5 Times FM.
Nikakumbuka siku hizo ambapo niliwa ndio kwanza nimevuka miongo miwili, Sister V alikuwa na SALIMIA USALIMIWE PARTY iliyowashirikisha wasikilizaji wa kipindi hicho ambao walikutana ofisi za Times kupanga mikakati ya kufanikisha "party" hiyo. Nikiwa natoka studio, mwenzangu niliyekuwa nafanya naye kipindi akaniita jina. Nikaitika anakinieleza aliloniitia na nilipoanza kuondoka Mama mmoja akaniuliza "wewe ndio Mubelwa Bandio?" Niliposema ndio akasonya kisha akasema "kumbe ni mtoto tu. Siku zote nakusikiliza nadhani mtu mzima zaidi yangu." Nikajichekelesha ki-unafiki na kuondoka.
Sasa haya mawili yamenifanya niwaze VIGEZO VYA UTOTO, UJANA NA UZEE NI VIPI?
Picha: Maisha na Mafanikio Blog
Ni kukua kwa uzazi ama? Kwani huyu binti anayesemekana kuwa na umri wa miaka 10 aliyejifungua ataendelea kuitwa mtoto? Je mtoto anaweza kuwa mtoto?
Ni uwezo wa kimaamuzi ama? Vipi kuhusu hapa Marekani ambapo kijana wa miaka 18 haruhusiwi kunywa pombe mpaka atimize miaka 21 (nadhani kwa uwezo wa kuamua akishalewa) lakini anaweza kupelekwa vitani akiwa kama askari ambako atafanya maamuzi ya kuua ama kutoua.
Ni muonekano wa mtu ama? Picha hizi zilipigwa mwaka mmoja. Kwani zote zaonesha "ujana" ulio sawia?
Ni mitindo ya mavazi na nywele ama?
Nasikia watu wakisema "yule naye miaka yaenda lakini mitindo yake ya nywele ama mavazi yake ama maongezi yake ni kama mtoto.
Ni muonekano wa mvi kama aliouliza Dada Yasinta hapa ama?

Ndio maana bado nawaza kuwa VIGEZO VYA UTOTO, UJANA NA UZEE NI VIPI?

6 comments:

ERNEST B. MAKULILO said...

Mzee wa Changamoto,

Nimeipenda sana hii mada yako. Kuna watu wengi nizungumzie kwenye tamaduni zetu Tanzania ambao huamini kuwa na busara ni kuwa na umri mkubwa. Sasa kutokana na article yako huyo msomaji wa blog na pia unayewasiliana naye kwenye facebook, alikua na ninadhani bado ana fikra kuwa busara ni umri mkubwa. Sasa anaposoma makala zako ambazo kusema kweli zinakuwa na ujumbe mzito, na kuonesha uwezo wa mtu anavyofikiria kwa umakini na kuwajali wengine, basi akajua wewe ni "mdingi" mzee sana. Kumbe sio hivyo. Na hata huyo dada aliyesonya, najua alidhani "ulipaswa" kuwa mzee kuwa na busara.

Binafsi "usumbufu" huo nimekutana nao sana. Mtu akikutana na muonekano wangu sometimes nywele yangu kuwa ndefu anasema ujana, utoto. Lakini wengine wanapokutana na blog yangu wanajua mimi ni "mdingi" hahahahaa.

MAKULILO, Jr.
www.makulilo.blogspot.com
San Diego, CA

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

zamani wazee walikuwa na busara au busara zilipimwa kukfuatana na umri na rafikiyo huyo alikuwa bado anaishi zamani

lakini hivi sasa wazee wamebakia kapa, hawana tena uwezo wa kujifunza kwa haraka kama vijana na mali/utajiri vimewekwa mikononi mwa vijana wanaoweza kujifunza fasta nakutumia teknolojia za kisasa zaidi

Sarp said...

Kaka Makulilo Umeongea kila kitu ambacho nilitaka kusema....U had a point

Baraka Mfunguo said...

Ukubwa, utoto na uzee upo wa namna nyingi. Mimi nadhani wapo pia vijana wanaowazidi wazee kwa kufikiri na ndio maana hata katika uongozi wetu Tanzania hilo limekwishajidhihirisha wazi. Kasumba imejengeka kwamba mtu anakuwa na busara akiwa mzee wakati ukiwa kijana ndio akili inachapa kazi uwezo mkuwa wa kufikiri na kutenda na hata kung'amua.

Nadhani kaka Mube huu mtazamo umekwishapitwa na wakati. Lakini natahadharisha pia katika hili kwamba Wazee wanatakiwa waheshimiwe na kuthaminiwa kwani inawezekana busara zao zinatokana na kiwango cha maisha waliyoyaishi na matukio waliyokumbana nayo pamoja na mafundisho yake. Na ndio maana waswahili wanasema " UKIMUONA NYANI MZEE UJUE AMEKWISHAKWEPA MISHALE MINGI.

Yasinta Ngonyani said...

Ni kweli mada nzuri sana. Ni kweli watu sijui wanaangalia nini katika hili kwani hata mie napata sana usumbufu kama nilivyoandika mara nyungi katika blog yangu kuwa huwa siruhusuwu kununu vitu bila kuonyesha kitambulisho, kama vile pombe nk. Na pia kama nataka kutafuta kadi wananiambia huruhusi mpaka miaka ..... na halafu pia kama nasafiri na basi basi nalipa nauli ya watoto. Yaani wanaangalia tu na kuona kuwa ni mtoto kweli hii haki? Ni swali zuri sana Vigezo vya Utoto, Ujana na Uzee ni vipi? nimelipenda hili swali.Upendo Daima

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Jamani ee, wengine si wazee bali tumekomaa tu kwa ajili ya matatizo!

Kila jamii ina vigezo vyake vya kupimia uzee na ujana. Vyetu nadhani vingi mmevigusia hapo juu. Tatizo linakuja pale tamaduni mbili au zaidi zinapogongana - kama vile ambavyo tunashuhudia sasa...

Kuna methali moja ya Kinaijeria inasema hivi "Wisdom does not reside in gray hair only" Nakubaliana nayo.