Thursday, July 22, 2010

Tuwaombao wanabana, sisi je? Kuna ajifunzaye???

Novemba 26 2009 niliandika bandiko lenye kichwa cha habari Nalinganisha majengo na uchumi wetu (irejee hapa) nikionesha tofauti kati ya bunge la Uingereza na Bunge letu. Nikaangalia muonekano na KIPATO cha nchi hizi na nikaishia kujiuliza maswali hayo.
Jana na leo kumekuwa na habari nyingine iliyonifanya nirejee kujiuliza kuhusu JUHUDI ZA WAHISANI WETU ukilinganisha na za kwetu.
Hivi karibuni tumesikia kuhusu nyongeza ya mishahara huko Kenya imfanyayo Waziri Mkuu kuondoka na zaidi ya theluthi ya pesa anazopata Waziri Mkuu wa Uingereza na pia asilimia kadhaa zaidi ya mshahara wa Rais wa Marekani.
Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe David Cameron
Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe David Cameron ambaye aliingia madarakani na kuanza kupunguza matumizi yasiyo ya lazima ya serikali. Aliahidi kufanya hivyo kwa vitendo baada ya kuamrisha kutoongezwa mshahara kwa baadhi ya watumishi.
Na wiki hii, David Cameron ameushangaza ulimwengu pale alipoamua kutotumia ndege ya kukodi wakati akifanya safari yake ya kwanza kubwa kikazi kuja hapa Washington DC kuonana na Rais Barack Obama. Katika safari hiyo, Waziri Mkuu huyo alitumia ndege ya abiria ya biashara (British Airways) na hivyo kuweza kupunguza matumizi ya zaidi ya $300,000 ambazo zingegharamia usafiri wa kawaida wa kukodi. Kwa mujibu wa Gazeti la The Sun la nchini Uingereza kama ilivyonukuliwa katika bandiko la leo katika Blog ya Jack Cafferty wa CNN, afisa mmoja wa serikali ya Uingereza amesema "When we are asking the country to tighten their belts as much as we are it's very hard to justify hiring big jets to swan around the world. It may make his travel a little harder, but the Prime Minister believes it's up to him to set an example."
Nimeshuhudia baadhi ya msururu wa viongozi wa nchi za Afrika (Tanzania ikiwa mojawapo) na ninawaza kama kuna watakalojifunza sasa.
Natambua Rais mmoja barani Afrika (sina hakika kama ni Zambia) aliamua kusitisha ndege ya Rais kupunguza gharama.
Pengine na sisi Tanzania kama tutafikiria hili na pengine kuongeza utendaji kazi wa MABALOZI ambalo litakata gharama za safari za kila uchao za Rais, naamini tunaweza kubaki na vi-senti vya kuchimbisha visima kadhaa vya maji kwa wananchi wanaohitaji saana, kujenga tu-vituo twa afya na mengine mengi.
Kwa ufupi ni kuwa TUACHE KUTUMBUA KULIKO WANAOTUWEZESHA KUWA NA MATUMBUZI HAYO.

No comments: