Friday, December 2, 2011

Truth Will Reveal.......Nasio Fontaine

"You see their faces but you never know their thoughts,
.. you see their actions but you never know their reactins,
Time and Time-alone will prove the story and every eye will see,
TRUTH WILL REVEAL"
NASIO FONTAINE
Photo Credits: Global Publisher
Nimekuwa kimya kuhusu sakata zima la KATIBA kwa kuwa nilihisi kilichokuwa kikiendelea kingekuwa MARADHI kwangu. Lakini leo nimeona nijikite kuoanisha DARUBINI hii ya mmoja wa wakali wa muziki wa reggae duniani na hili. Nakumbuka punde baada ya Mhe. Rais kutangaza kuwa mwaka huu utakuwa mwaka wa mchakato wa katiba, NILIHOJI HAPA kuhusu utekelezaji wa suala hili. Rais kwa kauli yake alisema ".. Jambo la nne ambalo tulilokubaliana kufanya ni kuanzisha mchakato wa kuitazama upya Katiba ya Nchi yetu kwa lengo la kuihuisha ili hatimaye tuwe na Katiba inayoendana na taifa lenye umri wa nusu karne." kisha akaendelea kusisitiza akisema "Ndugu Wananchi;
Ndiyo maana tukaamua kuanzisha mchakato huu na kwa ajili hiyo, nimeamua kuunda Tume maalum ya Katiba, yaani Constitutional Review Commission. Tume hiyo itakayoongozwa na Mwanasheria aliyebobea, itakuwa na wajumbe wanaowakilisha makundi mbalimbali katika jamii yetu kutoka pande zetu mbili za Muungano. Jukumu la msingi la Tume hiyo litakuwa ni kuongoza na kuratibu mchakato utakaowashirikisha wananchi wote bila kubagua, vyama vya siasa, wanasiasa, wafanyabiashara, asasi za kiraia, mashirika ya dini, wanataaluma na makundi mbalimbali ya watu wa nchi yetu kote nchini, katika kutoa maoni yao juu ya wayatakayo kuhusu Katiba ya nchi yao.
Baada ya kukamilisha kukusanya maoni,Tume itatoa mapendekezo yake yatakayofikishwa kwenye vyombo stahiki vya Kikatiba kwa kufanyiwa maamuzi.Baada ya makubaliano kufikiwa, taifa letu litapata Katiba mpya kwa siku itakayoamuliwa ianze kutumika.
Ndugu Wananchi;
Ni matumaini yangu kuwa mchakato huo utaendeshwa vizuri, kwa amani na utulivu kama ilivyo sifa ya nchi yetu na mazoea yetu ya kujadiliana bila kugombana. Wananchi watapewa fursa ya kutosha ya kutoa maoni yao kwa uhuru na pawepo kuvumiliana kwa hali ya juu pale watu wanapotufautiana kwa mawazo. Pasiwepo kutukanana, kudharauliana, kushutumiana, kubezana, kuzomeana wala kushinikizana. Naomba washiriki waongozwe kwa hoja badala ya jazba. Tukiwa na jazba, hasira na kushinikizana kamwe hatutaweza kutengeneza jambo jema. Na inapohusu Katiba ya Nchi itakuwa hasara tupu. Haitakuwa endelevu na kulazimika kufanyiwa marekebisho mengi mwanzoni tu baada ya kutungwa.
Nawaomba Watanzania wenzangu wenye maoni yao wajiandae kushiriki kwa ukamilifu katika mchakato huu. Katoeni maoni yenu mazuri yatakayowezesha nchi yetu kuwa na Katiba itakayokidhi matakwa yetu ya sasa na ya miaka 50 ijayo."
"
Na haya niliyapenda kwa kuwa yalisemwa kuoneysha kuwa YANGEHUSISHA wananchi kwa asilimia kubwa. Na hii ilikuwa ni hotuba ya kuuaga mwaka 2010 na kuukaribisha 2011. Japo sikukubaliana na wazo la tume, na Wizara na mengine kadhaa, nikaona ni vemakusubiri kitakachotoea. Na wiki hii tumeona madhara ya kuamini kauli za wanasiasa. Baada ya kile kilichoitwa "MAZUNGUMZO YA KIHISTORIA" baina ya Mhe. Rais Kikwete na viongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini CHADEMA, wengi waliamini kuwa kungekuwa na ushirikishwaji wa maoni ya wapinzani hao kwenye mchakato, hasa ikizingatiwa kuwa nao wana wafuasi wengi nchini na Rais alisema angependa kuona wananchi wakipewa "fursa ya kutosha" kutoa maoni yao.
Kilichofuata wote tunakijua. Hili tabasamu na muonekano wa "makubaliano" haukuakisi ukweli wa kilichotokea. Rais akatenda kinyume na mazungumzo yao, CHADEMA wakasema RAIS AMEWAUZA. Na katika kauli hiyo, Naibu Katibu mkuu wa CHADEMA Mhe. John Mnyika alikaririwa akisema "Kitendo cha Rais Kikwete kuusaini muswada huo bila ya kuupitia ni kinyume na makubaliano, jambo ambalo linatufanya tususie mchakato mzima wa kuuratibu maoni ya kwa ajili ya Katiba Mpya kupitia sheria ailiyoisaini,"
NINALOONA AMA KUELEWA NI KUWA Rais alitambua tangu awali kuwa hakuwa na mpango wa kubadilishwa mawazo na hiyo "kamati maalum" ya CHADEMA, lakini bado akaamua kukutana nao, kuchukua maoni yao na kuyaweka kando. Pesa ya wananchi ikatumika kuwakarimu Ikulu.
Kwa hiyo, USO WA RAIS HAUKUONYESHA KILICHO MOYONI mpaka maamuzi yalipotoka kuwa amesaini alichopelekewa, ambacho hakikuendana na kauli yake ya disemba 31, 2010.
Lakini NASIO mwisho ni mwa wimbo anasema "TUTAWAVUA HIZO MASK NYUSONI MWAO NA KISHA KUDHIHIRISHA UNAFIKI WAO.
Muda waja ambao tutajua ni nani aliye mtetezi wa wananchi. Kama ni Rais na mkakati wake wa katiba ama Chadema ambao nao yawezekana wanafanya UPINZANI tu na si kwa maslahi ya wananchi.
Msikilize NASIO FONTAINE katika wimbo huu...TRUTH WILL REVEAL
DONDOO: Sikia anavyoanza kwa KUWACHEKA hawa "wanafiki"

**Them, I & Them ni kipengele kikujiacho kila Ijumaa kinachoelezea kazi za wasanii (Them) kulingana na maono yangu (I) kwa ajili na manufaa ya hadhira (Them)**
Kwa nyimbo zaidi ndani ya kipengele hiki bofya hapa.

IJUMAA NJEMA

1 comment:

Ebou's said...

Hapo kamanda "bandio" sidhanikama kuna maslahi ya wananchi kama ijulikanavyo viongozi wa kiafrika wanafanya mambo mingi sana kwa maslahi yao wenyewe na sio ya wananchi Inauma sana, kwani wananchi ndio waliowaweka madarakani.

Tuombe M/Mungu tu Mh Bandio mchakato huo uendeshwe vizuri, kwa amani na utulivu/ M/mungu ibariki Tanzania na Watu wake Amin!